ACHANA na matokeo yaliyopatikana uwanjani kwenye dimba la Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, tujikite kwenye matokeo ya jambo husika! hapa tunazungumzia suala la kukumbukwa Jamii hususani kundi la Watoto waliokuwa kwenye Mahabusu pale Upanga kwa lengo la kuwarekebisha tabia.

Wapenda Soka, tumeona matokeo ya uwanja ya ushindi wa Team Kiba, ushindi wa jumla ya mikwaju ya Penalti 4-2 dhidi ya Team Samatta, baada ya sare ya bao 3-3 katika dakika 90, haijalishi! binafsi natoa pongezi kwa jambo walilofanya hawa jamaa, Msanii wa Bongo Fleva, Ali Saleh Kiba na Mwanasoka, Mbwana Ally Samatta.

Kabla ya mtanange huo wa hisani, tuliwasikia wakihamasisha kupitia ‘Foundation’ yao ya Samakiba kupitia mikutano na Waandishi wa Habari, kila mmoja kwa nafasi yake aliweka wazi kuwa Watoto hao watafurahi watakaposikia misaada mbalimbali imetoka kwa Samatta na Ali Kiba.

Kweli kabisa! wala hakuna ubishi kutoka na umaarufu wa Msanii Ali Kiba na Mwanandinga Samatta, Watoto hao watafarijika sana kupokea misaada hiyo, kutokana na wengine wengi kuwa na ndoto za kuwa Wasanii na hata wengine Wasakata kabumbu wakubwa ulimwenguni.

Nilimsikia Ali Kiba akizungumzia ndoto za baadhi ya Watoto hao, alisema wapo ambao wanatamani kuwa kama wao, ndio! swadakta wapo wenye ndoto za kuwa Wasanii wakubwa kama yeye, Wanasoka kama Samatta na wengine wanatamani kuwa Wasemaji na Wahamasishaji kama kina Haji Manara.

Bila shaka Kampeni hiyo itakuwa endelevu kila mwaka kuhakikisha jamii inasaidiwa ipasavyo kutokana na kuwa na uhitaji mkubwa, naamini kuna makundi mengi yenye uhitaji sio Watoto pekee.


PONGEZI KWENU SAMAKIBA

0713-017290



Post a Comment

Shasahn Media Group 2022.